
Mchezaji maarufu wa
soka nchini Brazil na ulimwengu kwa jumla Pele hayuko radhi kuondoka
nyumbani kwake kwasababu hawezi kutembea bila usaidizi , mwanawe
amesema.
Bingwa huyo mara tatu wa kombe la dunia, aliyejipatia
sifa za kuwa mchezaji bora zaidi wa kandanda alipelekwa hospitalini
akiugua maambukizi ya mkojo mwaka uliopita. Pele mwenye umri wa miaka 79 amekuwa na tataizo la nyonga yake kwa muda mrefu sasa na sasa anahitaji magongo ili kumsaidia kutembea huku shughuli zake nyingi za umma akizifanya akiwa katika kiti cha magurudumu.
''Anahisi aibu na anapendelea kujitenga na watu'' , mwanawe Edinho aliambia runinga ya TV Globo.
Pele alifunga jumla ya magoli 1,281 ikiwa ni rekodi ya duniani katika mechi 1,363 wakati wa kipindi chake cha miaka 21 katika kandanda , ikiwemo magoli 77 katika mechi 91 akiichezea Brazil.
Hali yake ya kiafya imekuwa ikitia watu wasiwasi katika miaka ya hivi karibuni na alifanyiwa upasuaji wa tezi dume 2015 baada ya kulazwa hospitalini kwa mara ya pili katika kipindi cha miezi sita.
"Fikiria, yeye ndiye Mfalme, alikuwa mtu wa kuvutia kila wakati na leo hawezi kutembea vizuri," Edinho alielezea.
''Anaona aibu hataki kwenda nje , hataki kuonekana ama kufanya kitu chochote kinachomtaka yeye kutoka nje. Ni dhaifu'' .
''Alifanyiwa upasuaji wa nyonga na hakupata muda mzuri wa kupona. Hivyobasi ana hili tataizo la kutembea kitu ambacho kimemsababishia shinikizo la kiakili''.
Mwezi Juni ataadhimisha miaka 50 tangu ashiriki katika kombe la dunia ambalo alishinda nchini Mexico na kile kilichoaminika na wengi kuwa timu bora zaidi duniani
0 comments:
Post a Comment