Meneja mpya wa West Ham David Moyes amesema kwamba anataka kutuma ujumbe fulani na kwamba anataka pia kujenga upya sifa zake katika klabu hiyo.
Meneja huyo wa zamani wa Everton na Manchester United alichukua nafasi ya Slaven Bilic, aliyefutwa Jumatatu klabu hiyo ikiwa eneo la kushushwa daraja kwenye jedwali.
"Nina jambo nahitaji kuthibitisha. Wakati mwingine inabidi kujaribu kukarabati mambo na nina mambo mengi nafaa kukarabati," amesema Moyes.
"Ni fursa nzuri kwangu, nimerejea na ndilo jambo ninalopenda kulifanya. Ninataka kufanya vyema na ninataka timu ifanye vyema pia."
Moyes, 54, amekuwa hana kazi tangu Mei alipojiuzulu wadhifa wake kama meneja wa Sunderland baada ya klabu hiyo kushushwa daraja.
"Ni jambo zuri kwa West Ham, wanampata meneja mzuri," amesema.
Moyes, ambaye alianza kazi ya umeneja Preston North End, alishinda tuzo ya Meneja wa Mwaka wa LMA mara tatu akiwa Everton kati ya 2002 na 2013.
Katika miaka 11 aliyokuwa nao, walimaliza katika nane bora mara tisa.
Alitia saini mkataba wa miaka sita kumrithi Sir Alex Ferguson katika Manchester United mwaka 2013 lakini akafutwa miezi 10 baadaye.
Moyes kisha alienda Uhispania na kuwa meneja wa Real Sociedad lakini akafutwa Novemba 2015 mwaka mmoja baadaye.
Alichukua hatamu Sunderland Julai 2016 lakini akajiuzulu Mei 2017 baada ya klabu hiyo kumaliza ikiwa inashika mkia Ligi ya Premia.
'Kibarua changu cha kwanza ni kushinda mechi'
Mechi zijazo za West Ham |
---|
19 Novemba: Watford (Ugenini); 24 Novemba: Leicester City (Nyumbani); 29 Novemba: Everton (Ugenini) |
3 Desemba: Manchester City (Ugenini); 9 Desemba: Chelsea (Nyumbani); 13 Desemba: Arsenal (Ugenini) |
West Ham wamo nafasi ya 18, baada ya kushinda mechi mbili pekee Ligi ya Premia msimu huu.
Walitumia jumla ya £42m majira ya joto kuwanunua wachezaji wakiwemo mshambuliaji Marko Arnautovic kutoka Stoke City kwa rekodi ya klabu ya £20m na mshambuliaji wa zamani wa Manchester United Javier Hernandez kutoka Bayer Leverkusen kwa £16m.
0 comments:
Post a Comment