NILIWAHI
kuandika mara kadhaa namna ambavyo wapenda mpira wa Tanzania wengi
tulivyo wanafiki na tunaovutiwa na kukurupuka katika mambo mengi
tusiyoyajua.
Nimewahi
pia kuelezea namna mashabiki wengi wa soka, tulivyo na tabia ya kuwa
wafuata mkumbo kwa kuwahukumu watu katika makosa ambayo tumesikia,
hatujachunguza wala kufanya angalau uchunguzi kidogo baada ya kusikia
lakini mwisho tunahukumu.
Huenda
anayesema ana jazba au anayesema ana chuki na mchezaji anayemsema, basi
ilimradi tu, basi tunaingia kama bendera fuata upepo na kulishikilia
bango.
Nasema
hivi wazi kuwa kwa wale wanaolia leo kuwa kipa wa Simba, Aishi Manula
anapaswa kuondolewa, wangependa kuona anayedaka ni Beno Kakolanya na
kigezo eti kwa kuwa Manula kafungwa mabao mawili dhidi ya Yanga.
Kati
ya wanaosema, hakuna anayethubutu kueleza kwa ufasaha akiyachambua yale
mabao mawili kiufundi kuturidhisha kuwa kweli ni makosa makubwa ya
Manula ambayo yanahitaji hukumu.
Hakuna
anayelalamika kuhusiana na aliyepokonywa mpira mguuni kabla ya
Mapinduzi Balama kuondoka nao, akionyesha alikuwa akitaka kupiga pasi
lakini akaachia mkwaju mkali ambao hakuna aliyeutarajia kulinagana na
sehemu aliyokuwepo lakini pia hata muonekano wa umbo lake.
Pamoja
na hivyo, anayesema Kakolanya adake, ana uhakika angeweza kuokoa shuti
hilo. Jaribu kutuliza akili, rudia mchomo huo matata wa Mapinduzi na
namna Manula alivyokwenda, sema tuone kama kweli ni kosa lake.
Vizuri
kufanya uchunguzi kabla ya kulalamika tu kwa jazba. Manula alifanya
kazi yake vizuri, nimejiridhisha, rudia ile video uone uhalisia. Acha
mihemko kwa kuwa tu umesikia na ukumbuke, Manula ni kipa na si ndege
mwenye mabawa, ulipokwenda mpira ni mara chache kipa kutokea kuuokoa na
inategemea aina ya mpira ulivyokwenda na position aliyopo, punguzeni
lawama tu bila kusifia.
Bao
la pili, Manula kafungwa na beki wake, nahodha wake Mohamed Hussein
Zimbwe ambaye alikuwa anajaribu kuokoa. Kwa kuwa Mohamed Issa ‘Banka’
alimsukuma kwa nyuma ilikuwa vigumu kwake kuwa na direction nzuri ya
kuupiga ule mpira.
Wakati
anasukumwa, Zimbwe akawa amepoteza uelekeo. Hivyo mpira ukaenda upande
wa Manula ambaye ulikuwa kama umemshitukiza, alijaribu kuuokoa ukamzidi
kasi.
Unamlaumu
aliyejaribu kuokoa wakati beki wake akimfunga? Ingekuwa lawama basi
aliyejifunga lakini katika mpira tunaamini alikuwa akijaribu kuokoa, ni
bahati mbaya, tunaocheza mpira tunasema bad lucky.
Sasa
iweje aliyejaribu kufuta kosa la aliyejifunga aonekane ndiye mwenye
makosa makubwa zaidi. Kama aliyejifunga mmeona ni bad lucky vipi
aliyejaribu kufuta kosa la mwenzake ikashindikana ndiye anaonekana
alikosea sana?
Kipa
hujiandaa sana anapoona mpira uko kwa mpinzani ingawa si asilimia 100
ndio ataokoa. Lakini inapotokea mpira uko upande wao, huamini ni salama.
Bila shaka Manula alijua Zimbwe anaokoa na yeye anatengeneza position
ya kuangalia kama kuna mpira utakaorudi tena aokoe, lakini anashtukia
tayari Zimbwe amepiga kichwa cha chini cha kushindilia, mpira unakuja
kwake kwa kasi.
Inawezekana
Manula akawa na makosa kama mchezaji lakini hastahili adhabu mnayotaka
kumpa na mkumbuke, mlifanya hivi kwa Kaseja, mkamlazimisha kuisha,
mkafanya aonekane mzee, sasa mmeanza kwa Manula.
Kawaida
sisi Watanzania hatupendi kuambiana ukweli, hatupendi kuwaona watu
fulani waking’ara kwa muda mrefu. Sasa Kaseja anawasuta wengi wenu
ingawa mmejikausha na wengine mmekuwa mstari wa mbele kumsifia kama vile
hamkushiriki kumzeesha kwa lazima.
Itakuwa
vizuri mkajipambanua mapema, ili siku moja Manula akiwa shujaa wa Simba
na taifa, basi tuwakumbushe kwa majina na kuwaonyesha mihemko yenu
haina faida.
Makocha
wa Simba wanajua wapi wanamhitaji Manula, wapi wanamhitaji Kakolanya na
ndio maana leo yuko Simba. Msiwashinikize wakaifanya kazi yao kwa
matakwa ya mashabiki badala ya weledi wa kazi yao, acheni mihemko,
acheni kulia na msivyovijua, mkiachiwa hivi, kesho mtasema Simba
imsajili Farouk Shikalo, kisa kaokoa sana dhidi ya Simba…halafu!

0 comments:
Post a Comment