Nahodha wa mabingwa
wa Uholanzi, klabu ya Ajax Matthijs de Ligt yupo safarini kuelekea mji
wa Turin Italia kukamilisha uhamisho wake na miamba ya Italia Juventus.
Inaaminika
kuwa Juventus watalipa kitita cha pauni milioni 67.5 kwa mlinzi huyo
stadi mwenye miaka 19 ambaye aliiongoza Ajax mpaka kwenye nusu fainali
za za Klabu Bingwa Ulaya msimu uliopita ambapo walifungwa na Tottenham. Beki huyo wa kati wa Uholanzi pia alikuwa akihusishwa na kuhamia klabu za Manchester United, Barcelona na Paris-St Germain.
Katika misimu yake mitatu na Ajax ametwaa ubingwa wa ligi ama maarufu kama Eredivisie na Kombe la Ligi, pia alikuwa kwenye kikosi kilichofungwa na Man Uited kwenye fainali za Kombe la Europa mwaka 2017.
De Ligt amefunga magoli nane katika mechi 77 za ligi alizoichezea Ajax.
Alijiunga na klabu ya Ajax akiwa na umri wa miaka tisa, na kukabidhiwa mikoba ya unahodha Machi 2018, akiwa ndiye mchezaji mdogo zaidi kupewa majukumu hayo klabuni hapo.

Alianza kuichezea timu ya taifa ya Uholanzi mwezi Machi 2017 baada ya kuichezea Ajax mechi mbili tu.
Uhamisho wa De Ligt ni jambo ambalo lilikuwa linatarajiwa toka kuisha kwa msimu uliopita.
Nahodha huyo hakuwa sehemu ya kikosi cha Ajax kilichosafiri kwenda nchini Austria kwa maandalizi ya msimu ujao.
Uongozi wa klabu hiyo ulitoa taarifa ya kuwa nahodha wao anabaki Amsterdam akisubiri kukamilisha uhamisho kwenda klabu nyengine.
0 comments:
Post a Comment